Google PlusRSS FeedEmail

MWENDESHA MASHITAKA NI MSHITAKIWA

Mwaka 1984, mkoani Dodoma ndani ya ukumbi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kulikuwepo kesi kubwa. Kesi ya kiongozi wa juu wa serikali ya Zanzibar. Alishitakiwa kwa kosa la kwenda kinyume cha “hati za Muungano” uliosainiwa na Abeid Amani Karume na Julius Nyerere.
Mtuhumiwa, Rais wa Zanzibar, hakuwahi kujiandaa vyema na kufikisha hoja yake mbele ya mamlaka ya Chama chake. Marafiki zake wa karibu walimuendea kinyume na kuiba waraka muhimu wa mashitaka katika shubaka la Ikulu. 

Bila shaka wale waliohusika walifanya wizi huu kwa siri kubwa kwani waraka wenyewe uliibiwa na kutolewa nakala na kurejeshwa ulipochukuliwa bila wahusika kujulikana. Waraka huo ukapelekwa Butiama kwa Mwalimu kwa ndege ya kukodi.

Njama hizo za kumwangamiza na kumtosa kiongozi huyo wa Zanzibar katika majanga ilikuwa ajali kubwa ya kisiasa na ya kihistoria  kutokea katika taifa letu. Mipango ikapangwa kesi ikadhihirishwa katika kikao cha Chama na kuwa kama mahakama. Mshitakiwa ni Rais wa Zanzibar. Akasomewa mashitaka yake yote mbele ya viongozi wenzake katika ukumbi wa Chuo cha CBE huko Dodoma. 

Mwendesha mashitaka dhidi ya Rais wa Zanzibar alijitokeza kwa haraka na kuona kama vile amepata bahati ya pekee. Sio mwingine ila alikuwa Maalim Seif. Akasimama kidete mbele ya hadhara na kuelezea kwa nini kiongozi huyo wa Zanzibar amefanya kosa na dhambi kubwa ya kutaka kuubadilisha muundo wa Muungano badala ya kuwa wa serikali mbili alitaka uwe wa serikali tatu kinyume na sera za Chama. 

Mwendesha mashitaka huyu kwa jasiri alijenga hoja zake za kutosha za kuonesha uzuri wa Muungano, tija ya Muungano wa Serikali mbili na kwa nini kiongozi huyo wa juu wa Zanzibar inapaswa achukuliwe hatua kali sana bila huruma!

Mwendesha mashitaka huyo akaungwa mkono sana na wafuasi wake akiwamo marehemu Shaaban Mloo. Mwendesha mashitaka huyo baadaye ikaonekana kuwa yeye ndiye aliyehusika mapema kuiba waraka huo katika shubaka au suraka ya huko Ikulu. 

Hivyo, basi alifanya kazi mbili za kuiba waraka na kumkabidhi Nyerere na kusimama kama mwendesha mashitaka namba moja dhidi ya Rais wake huyo. Mshitakiwa, Rais wa Zanzibar, kwa unyonge alikubali adhabu ya kujiuzulu kwa nafasi zake zote tatu. urais wa Zanzibar, makamu wa rais wa Tanzania na umakamu mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi.

Hakuruhusiwa kuishi Zanzibar. Viongozi wenzake wa karibu, wote wakafuata nyayo zake za kujiuzulu akiwemo waziri kiongozi wake. Viongozi wake waandamizi wakawekwa katika vifungo vya nyumbani katika mikoa kadhaa ya Tanzania Bara.

Matokeo yote hayo, mabaya kwa Rais wa Zanzibar na wenzake ni kazi “nzuri” ya kuiba nyaraka Ikulu na kusimamia kidete Mwendesha Mashitaka huyu stadi, bingwa, mahiri na jasiri - Maalim Seif. Ni bahati mbaya kuwa mwendesha mashitaka huyo ni mwanafunzi wa mshitakiwa katika Chuo cha Lumumba. 

Pia ni bahati mbaya mwendesha mashitaka alipewa nafasi ya masomo ya kwenda kusoma Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mshitakiwa. Ni bahati mbaya mwendesha mashitaka huyu alipewa kazi serikalini baada ya masomo na kumwingiza katika siasa na yeye mshitakiwa pia hata kufika nafasi aliyonayo sasa.  Hiyo ndio fadhila yake?  Hiyo ndio ahsante yake?  Ni bahati mbaya kuwa mwendesha mashitaka hivi sasa hayupo kizimbani kwa kutenda kosa na dhambi ileile aliyoifanya Rais wa Zanzibar aliyejiuzulu.Mwendesha mashitaka huyu aliyetetea Muungano wa serikali mbili kwa uchungu na hoja, leo amegeuka. Huyo ndiye leo anaongea hadharani kuwa sio tu anakataa serikali mbili bali anataka Muungano huo adhimu uliomfikisha leo hapo alipo uvunjwe kabisa.Yeye kama kiongozi wa juu na mtendaji mkuu wa chama chake anakwenda kinyume pia na sera ya Chama chake ya Muungano wa serikali tatu. Hivi mwendesha mashitaka huyu wa kesi kama hii kwa nini na yeye asishitakiwe na chama chake? Uadilifu wake uko wapi? Ukweli wake uko wapi? Sheria si msumeno? Unafiki na uzandiki umemtawala. Mwendesha mashitaka ni mshitakiwa, afikishwe kizimbani. Anayo kesi ya kujibu.
   CHANZO : Gazeti la Mzalendo Juni 30. 

This entry was posted in

Leave a Reply