Google PlusRSS FeedEmail

MAKAMU WA RAIS DKT. BILAL AZINDUA MRADI WA KUINUA UBORA WA ELIMU YA MSINGI 'TZ 21 CENTURY BASIC EDUCATION PROGRAM' MKOANI MTWARA.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiwaangalia na kuwasikiliza wanafunzi wa Shule ya Msingi Kambarage, walipokuwa wakijifunza kwa njia ya Kompyuta wakati alipofika shuleni hapo leo Juni 15, 2012, kwa ajili ya kuzindua Mradi wa Kuinua Elimu ya Msingi ijulikanayo kama 'Tz 21 Century Basic Education Program, mradi uliofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID). Kulia ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Shukuru Kawambwa (kushoto) ni Mtaalam wa Mitaala wa Mradi huo, Adrehem Kayombo. Picha na Muhidin Sufiani-OMR.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal amezindua Mradi wa Kuinua Ubora wa Elimu ya Msingi wa “TZ 21st Century Basic Education Program”  

Sherehe za uzinduzi wa mradi huo ambao unalenga kuinua ubora ya elimu ya msingi kwa kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano umeanzishwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID) zimefanyika leo katika shule ya msingi Kambarage mkoani Mtwara.

Akihutubia katika uzinduzi huo Dk. Bilal aliwataka Watanzania kuendelea kujenga imani na mfumo wa elimu uliopo nchini kwani ni mfumo bora ukilinganisha na mifumo ya elimu iliyopo katika nchi nyingine za Kusini Mashariki mwa Afrika.

Makamu wa Rais alisema kwa muda mrefu sasa, imani imejengeka katika jamii kwamba elimu inayotolewa hapa nchini ni duni na inahitaji kubadilishwa.

Aliwahakikishia Watanzania kuwa elimu inayotolewa hapa nchini haijashuka kiasi hicho kwani matokeo ya Utafiti wa Kufuatilia Ubora wa Elimu katika nchi za Kusini Mashariki mwa Afrika (SACMEQ) ya mwaka 2000 na 2007 yanaonyesha kuwa ukilinganisha na nchi nyingine, mfumo wa elimu hapa nchini ni bora.

“Kwa mfano, kati ya nchi 15 zilizofanya utafiti huo, nchi yetu ilifanya vizuri katika somo la Hisabati na Kusoma na kuwa kati ya nchi bora za kwanza katika utafiti wa mwaka 2007,” alidokeza Dkt. Bilal.

Makamu wa Rais pamoja na kukiri kwamba kuna watoto wachache wanaomaliza darasa la saba bila ya kuwa na stadi za kusoma na kuandika vizuri lakini alisema wapo wengi wanaomaliza na kufanya vizuri na kuwasihi wananchi wasikatishwe tamaa na maoni ya watu mbalimbali kuhusu kushuka kwa elimu nchini bali waongeze juhudi na kuwa na fikra chanya katika kutoa elimu bora.

Dkt. Bilal alitumia fursa hiyo pia kuwataka wadau wa elimu kulipa umuhimu wa pekee suala la upimaji na utahini katika shule za msingi kwani mitihani bora bado ni changamoto ambayo inahitaji kuangaliwa upya na wazazi na walimu kwa upande wao wana jukumu la kuhakikisha watoto wanasoma maana elimu bora ya msingi ndiyo itakayosaidia kuondokana na umaskini na kuwa na maendeleo endelevu.

Akizungumza katika hafla hiyo Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dkt. Shukuru Kawambwa alisema mradi huo utasaidia katika kufanikisha utekelezaji wa MMEM Awamu ya III (2012-2016) hususan katika kuinua kiwango cha ubora wa elimu ya msingi itolewayo nchini.

Naye Balozi wa Marekani nchini Alfonso Lenhardt alielezea kufurahishwa kwake kwa kuingizwa mradi huo katika utaratibu wa kutoa taarifa za elimu (Education Management Information System) akiwa na matumaini kwamba utasimamiwa na kuendelezwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiwaangalia na kuwasikiliza wanafunzi wa Shule ya Msingi Kambarage, walipokuwa wakijifunza kwa njia Kompyuta wakati alipofika shuleni hapo leo Juni 15, 2012, kwa ajili ya kuzindua Mradi wa Kuinua Elimu ya Msingi ijulikanayo kama 'Tz 21 Century Basic Education Program, mradi uliofadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID). Kushoto ni Balozi wa Marekani nchini, Alfonso Lenhardt, (wa pili kushoto) ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Shukuru Kawambwa, (kulia) ni  Mtaalam wa Mitaala wa Mradi huo, Adrehem Kayombo. Picha na Muhidin Sufiani-OMR

This entry was posted in

Leave a Reply